MGOMBEA UBUNGE ACT-WAZALENDO ILALA AHAIDI KUWA SAUTI YA WANYONGE
Na Mwandishi Wetu
MGOMBEA Ubunge wa Jimbo la Ilala kupitia Chama cha ACT-Wazalendo, Friday Yachitwi ametangaza rasmi azma yake ya kuwa mtetezi wa wanyonge kwa wafanyabiashara wadogo ikiwa atapewa ridhaa na wananchi kuwa mwakilishi wao katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Akizungumza mara baada ya kurejesha fomu ya uteuzi, mgombea huyo alimshukuru Mungu na Tume huru ya Taifa ya Uchaguzi kwa kumpa nafasi hiyo, akisema sasa "wanyonge wamepata mkombozi."
“Ilala si jimbo tu, ni mlango ambao Mungu amenipitishia kuitetea dunia. Hili ni jiji la biashara, kituo kikuu cha biashara Afrika Mashariki na Kati. Nitakuwa sauti ya wafanyabiashara na walalahoi,” amesema
Aliahidi kuwa kipaumbele chake kikuu ni kuwalinda na kuwatetea wamachinga, bodaboda, na askari mgambo ambao wamekuwa wakifanya kazi kubwa kwa mazingira magumu, bila malipo stahiki.
“Hakuna machinga atakayenyang’anywa mali zake kama mimi nitakuwa Mbunge. Migambo na kina mama wa usafi barabarani wanapaswa kulipwa mishahara ya kutosha kwa kazi wanayoifanya,” ameongeza
Pia aligusia changamoto katika huduma za afya akitolea mfano wa Hospitali ya Taifa Muhimbili na Amana ambazo zipo ndani ya Jimbo la Ilala.
Aliahidi kupigania wananchi kupata matibabu bila bugudha, na kuhakikisha maiti au wagonjwa hawazuiwi kwa sababu ya kushindwa kulipa bili.
“Nina nia thabiti ya kuleta mabadiliko. Wananchi wa Ilala naomba mniamini, mnikabidhi dhamana ili niwe sauti yenu ya kweli bungeni,” amesisitiza


Comments
Post a Comment