TARURA YABORESHA MIUNDOMBINU KUKABILIANA NA ATHARI ZA MABADILIKO YA TABIANCHI
Na Mwandishi wetu
SERIKALI kupitia Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) inaendelea kuimarisha usimamizi wa mazingira kwa kujenga miundombinu thabiti ikiwemo madaraja ili kukabiliana na athari za mafuriko yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi.
Hayo yameelezwa na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu–TAMISEMI (Miundombinu), Mhandisi Rogatus Mativila katika Mkutano wa 30 wa Umoja wa Mataifa kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (COP 30) unaoendelea jijini Belem, Brazil.
Mhandisi Mativila amesema Mpango wa ‘SCALE’ (Scaling up Locally Led Climate Actions) unaoanza kutekelezwa kupitia fedha za mkopo nafuu kutoka Benki ya Dunia ni muhimu katika utekelezaji wa Mkakati wa Taifa wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa kuwa unahusisha jamii husika katika maeneo yao ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Ameeleza kuwa mpango huo unatarajiwa kuwafikia watu takribani milioni 6.6 katika mamlaka 65 za Serikali za Mitaa zikiwemo 54 kutoka Tanzania Bara na 11 kutoka Zanzibar, na umeongeza nguvu katika ujumuishwaji wa makundi maalumu kama vile wanawake na vijana.
Aidha, amesema TARURA na DART zinaendelea kuwa nguzo madhubuti katika ujenzi wa miundombinu yenye ustahimilivu kuanzia ngazi za jamii na katika kuboresha fursa za kiuchumi kwa wananchi.

Comments
Post a Comment